Wasalaam wapenzi wa soka nchini,Hatuna budi kuwa na furaha kutokana na muelekeo wa soka letu hasa ukilinganisha na nchi jirani kama Kenya na Uganda hata Rwanda ambapo utaona soka letu Tanzania linakua kwa kasi ndio maana kila siku mijadala kuhusu soka inaongezeka na hapo ndipo ukweli wa uelekeo chanya wa soka letu unapoonekana maana mashabiki wamehamasika kufuatilia soka hata baada ya mechi kuisha wamebaki wanalizungumza.
Hivi karibuni baada ya sarakasi za usajili Kiungo Benard Morrison alifanikiwa kujiunga na klabu ya Simba sc na alianza na moto katika mechi za ya kirafiki dhidi ya Vital O ambapo alifunga na kutoa pasi ya goli huku pia timu nzima ya Simba sc ikionyesha soka safi.
Baada ya hapo ilikuja mechi ya ngao ya jamii baina ya Simba sc dhidi ya Namungo Fc ambapo bado staa huyo alionyesha kwanini Yanga sc imekimbilia Fifa baada ya kucheza kwa kiwango kikubwa na kufanikiwa kufunga na Kutoa penati iliyofungwa na nahodha John Boko.
Mechi iliyofuatia dhidi ya Ihefu na dhidi ya Mtibwa Sugar ndio zimezua mjadala kuhusu kiwango cha staa huyo raia wa Ghana ambapo katika mechi hizo hakufurukuta kiasi cha kocha Sven kuamua kufanyia mabadiliko ya mapema kipindi cha pili na hapo ndipo mashabiki wa soka hasa wa Yanga sc wameanza kumbeza wakichagiza na historia ya wachezaji kadhaa waliohama Yanga sc na kwenda Simba sc ambapo hawakucheza kwa viwango wakiwaorodhesha Haruna Niyonzima,Ibrahim Ajibu na Gadiel Michael.
Je Kiwango Kimeshuka?
Nachelea kukubaliana na hilo kwa sababu wazungu husema “Form is temporary but class is Permanent”kwa maana kwamba hakuna ubishi kwamba Morrison ni mchezaji wa daraja la juu kwa hapo nchini katika ligi yetu kutokana na kuwa na sifa za kipekee hasa akiwa na mpira mguuni hukimbilia ndani ya eneo la 18 kitu ambacho mawinga wengi hapa nchini hawana.
Pia Utulivu wa Morrison akiwa na mpira ni hali ya juu hasa akiingia ndani ya box ambapo huweza kufunga yeye mwenyewe pia sio mchoyo wa kutoa pasi ya mwisho kama alivyofanya katika mechi dhidi ya Vital O utulivu huo pia huweza kusababisha penati kama ilivyokua dhidi ya Namungo.
Uwezo wa kucheza mipira iliyokufa pia ni silaha kwa winga huyo mwenye mbio ambapo kama unakumbuka lile bao alilomfunga Aishi Manula nje ya box wakati akiwa Yanga sc ni ushahidi tosha kuhusu uwezo wake huo.
Nini Kimesababisha Asifanye Vizuri katika Mechi Hizi Mbili
Mosi ni mbinu za walimu wa timu pinzani ambazo zimecheza na Simba sc katika michezo hiyo miwili ya egenini za kuamua kuanza kuikabia Simba sc kuanzia juu hivyo kutowaruhusu kufanya Build up ambazo zingewafanya Simba kupanga mashambulizi wakiwa wamerelax badala yake kitendo kuwakabia juu kuliwafanya kina Morrison,Chama na Miqquisone kutumia muda mrefu kushuka chini kuomba mipira na hata walipoipata walikua mbali na goli huku wachezaji wa Mtibwa wakiwa wameshaziba nafasi za mikimbio ikumbukwe walikabwa na mawinga wa pembeni wa Mtibwa na Mabeki wa pembeni waliokuja kufanya Clearance tu pale mawinga walipozidiwa.Tuwape kongole sana Zubeiry Katwila na Maka Mwalwisi kwa hilo.
Pili ni viwanja vilivyotumika haviruhusu soka la falsafa ya Simba ya kukimbia na mipira huku wakitafuta nafasi kupitia mashimo yanayopatikana hivyo kupata magoli zaidi kupitia njia za pembeni na hili nategemea katika mechi ijayo dhidi ya Biashara ambapo winga za Simba zitafanya vizuri zaidi kutokana na uwanja kuruhusu mikimbio.
Tatu,Mwalimu Sven ndo wa kulaumiwa kutokana na kulazimisha mfumo mmoja tu licha ya wakati mwingine kumpa changamoto ya kuwa na mshambuliaji mmoja.Ingependeza hasa mikoani atumie washambuliaji wawili Kagere na Boko huku silaha yake iwe kupiga mipira ya juu ndani ya Box la timu pinzani hili lingempa matokeo kwa urahisi zaidi kupitia vichwa na mipira ya Rebound.
Wasalaam,
Maniche Mayaya