Kikosi Maalumu cha Kuzuia Magendo Zanzibar (KMKM) kimempandisha cheo nyota wa timu ya Yanga Sc Ibrahim Hamad “Ibra Bacca” kutoka Koplo na kuwa Sajenti kutokana na kuonesha kiwango bora kwenye mchezo wa soka.
Bacca amepandishwa cheo hicho Visiwani Zanzibar mbele ya mabosi wa jeshi hilo wakiongozwa na mkuu wa kikosi hicho Comodore Azana Said Msingiri.
Beki huyo amepandishwa cheo hicho kutokana na kuonyesha kiwango kizuri akiwa katika klabu yake ya Yanga Sc pamoja na timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars).
“Ukifanya kitu kizuri basi ni Wajibu wangu kama mkuu wa kikosi sina budi kutoa pongezi kutokana na kuiwakilisha vyema jeshi katika kazi anazozifanya katika klabu yake ya Yanga Sc na timu ya Taifa”,Alisema Msingiri.
Kwa upande wake mchezaji huyo alishukuru jeshi hilo kutokana na kuutambua mchango wake tangu ajiunge na klabu ya Yanga sc.
“Sina budi kushukuru kikosi changu kwa kuweza kunisapoti kwa kila hatua. Nitaendelea kuipambania nchi yangu,” amesema Sajenti Ibrahim Bacca ambaye wazazi wake pia ni askari.
KMKM iliyomwachia Bacca kuitumikia Yanga sc tangu mwaka 2022 ni kikosi cha ulinzi cha Zanzibar ambacho kina jukumu la kulinda mipaka ya bahari dhidi ya magendo, uvuvi haramu, na vitendo vingine vya kihalifu. Pia KMKM husaidia katika operesheni za uokoaji baharini na usalama wa majini.