Kampuni ya michezo ya kubashiri ya SportPesa imeashiria inapanga kurejea katika soko la Kenya, saa chache tu baada ya Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta kusaini mswada wa fedha Juni 30, 2020 .
Baada ya serikali kulegeza msimamo wake hapo Juni 30 kuhusu ushuru wenye utata unaotozwa kampuni hizo na watu wanaobashiri mechi na ambao ulichangia kampuni nyingi kujiondoa soko la Kenya, SportPesa ilichapisha ujumbe kwenye mtandao wake wa Twitter wa kupatia wateja wake matumaini .
Ikijibu mteja AChevinar aliyeuliza kama itarejea Kenya, SportPesa ilisema, 🗣️“Hatuna tarehe rasmi tutakayorejelea shughuli zetu, lakini tuna matumaini ya kufanya hivyo.”
Mswada huo, ambao umefanyiwa marekebisho, unaondoa ushuru utata uliochangia SportPesa na ile ya Betin na nyinginezo kujiondoa Kenya miezi tisa iliyopita .
Kabla ya kujiondoa kabisa katika soko la Kenya mnamo Septemba 2019, SportPesa ilikuwa ikidhamini Gor Mahia, AFC Leopards, Ligi ya Ndondi, Shirikisho la Raga Kenya, Kenya Harlequin, Ligi Kuu ya Soka ya Kenya na pia mashindano ya kimataifa kati ya klabu za soka za Kenya na Tanzania pamoja na kuleta klabu ya Uingereza Everton nchini Kenya na Tanzania na Hull City nchini Kenya, miongoni mwa shughuli zingine. Pia, ilikuwa imeajiri mamia ya Wakenya katika afisi zake jijini Nairobi .
SportPesa ilikuwa mstari wa mbele kupinga sheria kali za kutozwa ushuru wa asilimia 35 zilizopitishwa na serikali. Kampuni hiyo inasemekana ilikuwa ikipokea Tsh. bilioni 434 kila mwezi kutokana na beti ambazo Wakenya walikuwa wakiwekeza wanapobashiri mechi za Kenya na mataifa mengine, wakitafuta kujishindia fedha .
Kampuni hiyo, ambayo ilianza shughuli zake Kenya mwaka 2014, ilikuwa ikitawala asilimia 64 ya soko la humu nchini. Ilisalia na katika mataifa ya Tanzania, Afrika Kusini, Italia, Ireland, Isle of Man na Uingereza baada ya kujiondoa Kenya.Betin inaaminika ilitawala soko la Kenya kwa asilimia 20 ikifuatiwa na Betika, Betpawa Sportybet .
Cc:Adam Salamba/Mitandao