Klabu ya Yanga sc imefanikiwa kufuzu hatua ya nusu fainali ya kombe la Muungano nchini baada ya kuifunga timu ya Kvz kwa mabao 2-0 katika mchezo uliofanyika katika uwanja wa Gombani Visiwani Pemba usiku ya Aprili 26 2025.
Kocha Miloud Hamdi aliwapumzisha mastaa wake Djigui Diarra,Prince Dube na beki Ibrahim Hamad Bacca lakini kutokana na kuwa na kikosi kipana klabu haikutetereka baada ya kupata bao la kwanza kupitia kwa Stephan Aziz Ki aliyecheza kama mshambuliaji wa kati baada ya kupokea pasi ya Dennis Nkane dakika ya 28.
Kvz waliendelea kukaba kwa umakini na nguvu kubwa ili kuzuia mvua ya mabao lakini Yanga sc walicheza wakiwa wamerelax na kufanikiwa kufunga bao la pili dakika ya 88 lililofungwa na Nkane baada ya mabeki wa Kvz kufanya makosa kutokana na kukabwa kwa nguvu (Pressing).
Kutokana na ushindi huo sasa Yanga sc wamefuzu hatua ya nusu fainali ya michuano hiyo maalumu kuadhimisha miaka 61 ya muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambapo watavaana na Zimamoto Fc siku ya Aprili 29 2025.